Sunday, October 28, 2012


HOFU YA VITA VYA KIENYEJI NGORONGORO,WAALIMU ,WANAFUNZI WAKIMBIA,

SERIKALI YAAHIDI KUTATUA MZOZO BAINA YA WASONJO NA WAMASAI  

Mwandishi wetu Loliondo


WAALIMU na wanafunzi wa shule ya msingi Nan  katika kata ya Engusero Sambu  Wilayani Ngorongoro Mkoani Arusha wamekimbia  shule hiyo kutokana na hofu ya kuvamiwa na kuuawa kwa sialaha za moto zinazodaiwa kumilikiwa na jamii za kisonjo na kimasai ambazo zimekuwa zikipigana mara kwa mara.

Shule hiyo ina wanafunzi  248 kati yao wavulana 158 na wasichana 100.
Hivi karibuni watu wanaodhaniwa kuwa ni vijana wa Kisonjo   wakidaiwa na sialaha za moto walivamia katika eneo hilo na kupora mifugo na kujeruhi watu
 kadhaa kwa risasi.

Waalimu hao ambao hawakutaka kutajwa majina yao   waliwaambia waandishi wa habari kuwa tetesi za morani wa kimasai kuvamia maeneo ya wasonjo kulipiza kisasi zimezagaa katika eneo hilo na kwa hiyo hawawezi kufanyakazi katika mazingira hayo.

“Hatutaki kutaja majina yetu tutapata matatizo ,Hata wanafunzi hawapo tutafanya kazi gani hapa ,serikali imeshindwa kumaliza migogoro ya jamii hizi na sisi  tunakuwa wahanga”alisema Mwalimu mmoja wa shule hiyo.

Walisema kuwa hata wanafunzi wa darasa la saba walilazimika kuhamishwa kwenda kufanya mitihani wa kumaliza elimu ya msingi katika eneo la Wasso kutokana na hali ya usalama kuwa tete.

“Unajua katika tukio hilo mtu mmoja aliuawa mashine ya kusaga nafaka kuchomwa moto na mamia ya mifugo ya wamasai iliporwa na watu hao ambao wanadaiwa kutumia silaha za kivita ikiwemo AK47 na SMG”alisema mkazi wa Kisangiro
Alieleza kuwa baadhi ya watoto wamebaki majumbani miezi miwili na kama serikali haitawafuatilia hiyo ndio itakuwa njia ya wazazi kukwepa jukumu la kuwasomesha.

Naye afisa elimu shule za msingi Wilayani humo Papaa Kinyi alithibitisha kuwepo kwa hali na kusema kuwa wanajaribu kuwashawishi waalimu hao kurudi shule kwa kuwa vyombo vya ulinzi na usalama vinafuatilia hali ya mambo katika eneo hilo

“Ni kweli Waalimu wana hofu lakini serikali inafanya kila linalowezekana kurejesha amani katika eneo hilo”alisema Papaa Kinyi.

Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro Elias Lali alisema kuwa serikali inaendesha zoezi la kupokonya silaha za moto kutoka kwa watu wanaozimiliki kinyume na sheria.
Alisema hadi kufikia sasa wamekwisha kamata bunduki mbili aina ya SMG na Riffle na kwamba zoezi bado linaendelea.

“Ni kweli hapa kuna hofu kutokana na uvumi unaoendelea lakini vyombo vya usalama viko tayari kukabili tishio lolote la usalama ,tunajaribu kuhamasisha waalimu na wazazi kuwarudisha watoto kuendelea na masomo”alisema Lali
Alieleza kuwa serikali iko mbioni kupeleka msuluhushi wa mipaka ili kumaliza migogoro yote ya ardhi katika Wilaya hiyo.

"Msuluhishi huyo atateuliwa na wizara ya ardhi na tunaamini kuwa hili tatizo la mipaka likishughulikiwa vizuri hii migogogro na vita vitaisha hapa"alisema Lali
Eneo la Loliondo limekuwa likikumbwa na vurugu za kikabila mara kwa mara   baina ya wasonjo na wamasai  ambapo watu zaidi ya ishirini  wamekwisha poteza maisha katika kipindi cha miaka 15 iliyopita.

kwa upande wao wasonjo wandai kuwa serikali imekuwa ikiwapendelea Wamasai na kuwapa haki zaidi katika mizozoz inayotokea katika eneo hilo yakihusisha ugomvi wa mipaka ya maeneo ya malisho na mifugo  baina jamii hizo

indaiwa kuwa wananchi wengi wa jamii hizo wanamiliki silaha za moto ambazo zinaelezwa kuingizwa na Wasomali katika miaka ya hivi karibuni kabala ya kuondoshwa na jeshi la wananchi wa Tanzania.  

0 comments:

Post a Comment

Time Management

Translator

Popular Posts

Blog Archive

Fellow Bloggers

Popular Posts

Visitors Worldwide

Total Pageviews